UJANA
Umuhimu wa ujana
Ujana ni hatua kubwa ya maisha
ambayo kwa maisha ya mwanadamu ndio hatua ndefu yenye mambo mengi, na katika
hatua hii nguvu na hisia hutawala lakini pia changamoto za maisha huibuka kwa
wengi (mithali 16:9). Hatua ya ujana ni umri wa mtu kufanya maamuzi hivyo
hekima inastahili kutumika kuliko nguvu na hisia/hulka (mhubiri 10:10, mithali
9:10) hapa ujana unahusisha wa kike na wakiume na wito ni huu “kumcha Mungu”
wakati wa ujana “kumcha Mungu ni mwanzo wa hekima” (mithal 2:6, mithali 9:10,
mithali 5:1-12, mithali 31:30)
Hekima ya Mungu isipotuongoza
katika ujana ni ngumu katika uzee kuipata (mhubiri 4:13). Pia tukumbuke
binadamu wote tunazaliwa na ujinga mioyoni mwetu hivyo katika ujana ni hatua
pekee ya kuweza kuushinda ujinga (mithali 22:15).
Hatua
za maisha
Hatua kubwa za maisha zipo
katika maeneo makubwa matatu utoto, ujana na uzee.
(i)
Eneo la utoto
ni hatua ya kwanza na kiukweli
ujinga ndio hutawala moyo wa mtoto (mithali 22:15, mithali 23:13-14) hatari ya
ujinga ukikomaa huwa uovu hivyo kiboko, adhabu, na mafundisho ya Yesu Kristo ni
haki kwa mtoto (1yohana 2:28). Maana hekima kwa mtoto huwa ni furaha kwa mzazi
(mithali 23:15-16)
Ujinga ni jumla ya mambo yote mtu
anayofanya pasipo fahamu nzuri ya maadili kwenye jamii, mambo hayo hutokana na
tamaa/hisia/hulka (matakwa ya mwili) (wagalatia 5:17,19-21, 1yohana 2:16,
1yohana 2).
(ii) Eneo la ujana
Ni hatua inayohitaji kumcha
Mungu sana ili kupata hekima na neema yake kuliko kuendelea kufuata mambo ya ujinga
(mhubiri 12:1, mithali 9:10). Yesu kristo Mwenyewe alikua kwa kimo na hekima
huku akimpendeza Mungu na wanadamu toka utotoni (luka 2:40,52).
Moyo wa mwanadamu hufanyika
sehemu ya ibada ya kipekee tena ni sadaka kwa Mungu; ajabu ni kwamba moyo
huharibiwa sana na mawazo ya uovu ya kumwasi Muumba kwenye umri wa ujana
(mwanzo 8:21, yeremia 17:9-10, mithali 20:5). Hii ndio sababu Yesu Kristo
anasema nipe Moyo wako (mithali 23:26,) pia mpende BWANA Mungu wako kwa Moyo
wako wote (kumbukumbu 6:5) kwa roho yako yote na kwa nguvu zako zote. Tena
wenye hekima walisema ‘mtumaini BWANA kwa moyo wako wote wala usitegemee akili
zako mwenyewe (mithali 3:5) mkiri yeye, naye atanyosha mapito yako’ (mithali
3:6)
Neno la Mungu linashauri sana
kulinda moyo kuliko yote tuyalindayo maana ndiko zitokako chemchem za uzima
(mithali 4:23). Kama Mtu umeshindwa kuulinda moyo wako ungependa nani asaidie
kuulinda Yesu kristo au ibilisi (mithali 13:3), kama ni kristo jua unatakiwa
uyahifadhi maneno yake ushike amri zake ili uishi (mithali 4:4, mithali 14:33)
ndipo atakapo kuja na kuishi na wewe (yohana 14:23-24)
BWANA akiwa pamoja nawe,
unakuwa mfano wa shujaa mwenye kutisha, kwa hiyo hao wanaokuonea watajikwaa
wala hawatashinda; watatahayarika sana. Kwa sababu hawakutenda kwa akili,
wataona aibu ya milele ambayo haitasahauliwa kamwe (Yeremia 20:11).
Katika ujana endapo moyo wako
utatumainia akili au nguvu au mtu au vitu kama mali, vyote hivi vitavunja moyo
wako maana ndiyo hatma yake. Hakuna mwanadamu anaeweza kusaidia moyo wa mtu
ukivunjika wala hakuna anaeweza kustahimili (mithali 18:14). Na ndio kusudi
Mungu alimtuma Mwanae Yesu Kristo ili aje duniani kuganga waliovunjika moyo, na
kuwatangazia mateka uhuru wao (isaya 61:1).
Moyo ni kitu cha thamani kwa
Mungu ndio sababu alimtuma Yesu Kristo aje ulimwenguni kurudisha kile
kilichopotea, yaani moyo uliokengeuka. Kwa moyo tunampenda (kumbu 6:5), kwa
moyo tunaamini (warumi 10:10), kwa moyo tunamtii (mithali 4:4), kwa moyo
tunamtumaini (mithali 3:5)
(iii)
Eneo la uzee
Hii ni hatua ya mwisho ya
maisha, hapa kuna uzee mwema na uzee mbaya ila katika uzee ni wakati wa
kumbukumbu za ujana. Mtu anaweza kupata majuto au furaha ikitegemeana na hatma
anayoiendea au na jinsi alivyoishi ujanani.
Maoni
Chapisha Maoni