KUTAMBUA NJIA YA MAISHA TUNAYOPITIA


Isaya 48:17 ”BWANA, Mkombozi wako,mtakatifu wa Israel, asema hivi; Mimi ni BWANA, Mungu wako, nikufundishaye ili upate faida, nikuongozaye kwa njia ikupasayo kuifuata”
Wengi tunaishi duniani pasipo kufahamu njia tunayotakiwa tupitie hii hutufanya hata katika majaribu madogo tuanguke kwa kukata tamaa, kuvunjika moyo na hata kuangamia. Haya yanatupata  katika Nyanja tofautitofauti za maisha kama ndoa, urafiki, kazi, familia, masomo, na hata katika umiliki wa mali. Tukiwa hatutambui njia tuipitayo ni rahisi kuangukia kwenye utumwa, na vifungo vya ibilisi mpaka mauti. Mithali 14:12 “Iko njia ionekanayo kuwa sawa machoni pa mtu, Lakini mwisho wake ni njia za mauti”.
Binadamu tunamahangaiko mengi hasa katika kutafuta mafanikio, kujenga mahusiano, na hata kutafuta nguvu katika jamii. Watu wengi wanamali nyingi, elimu kubwa, wake/waume wazuri, marafiki wema tena maarufu lakini bado hawatembei katika njia iwapasayo. ”Nitakufundisha na kukuonyesha njia utakayoiendea; Nitakushauri jicho langu likikutazama” (Zaburi 32:8). Mungu pekee huwaonyesha watu wapi pa kupita maana kila mmoja aliumbwa katika mpango wake na malengo yake na kwa njia moja tu ya imani watu wanapata nafasi ya kusikia shauri na maelekezo ya Mungu na hivyo kutii na kufuata makusudio ya Mungu. Hiyo ndiyo njia impasayo mtu kuifuata.
Wengi wanashindwa kuelewa wanaposoma Yohana 14:6 isemayo, “Yesu akamwambia, Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi”. Huu ni mstari  muhimu sana kwa kila Binadamu yaani, kale kabla ya kuja kwa Yesu watu walifikia Uzima na kwa Baba kwa kushika torati (ila hata ivyo ni wachache sana wanaoweza kuitimiza sheria) lakini baada ya Yesu kuja watu hufikia uzima na kwa Mungu kwa kumuamini Yesu mwenyewe ndiyo maana anasema “Mimi ndimi njia” yaani tukimwamini Yeye katika kweli yake tutafika kwenye Uzima wa Mungu
Zipo njia zinazoonekana ngumu kwetu lakini ndio mpango wa Mungu na kuna njia rahisi mno lakini tunakuwa tumepotea. Ajabu ni kwamba kuna wakati tunakuwa na mipango mingi ambayo ni halali na mingine si halali ambayo nayo inatakiwa ithibitishwe na Mungu Mwenyewe.

Mithali 16:1-4 imeeleza kwa mapana kwamba “maandalio ya moyo ni ya mwanadamu; Bali jawabu la ulimi hutoka kwa BWANA. Njia zote za mtu ni safi machoni pake mwenyewe; Bali BWANA huzipima roho za watu. Mkabidhi BWANA kazi zako, Na mawazo yako yatathibitika. BWANA amefanya  kila kitu kwa kusudi lake; Naam, hata wabaya kwa siku ya ubaya. Mistari hii inatupa hitimisho kuwa maisha bila Yesu hakuna tunapoenda zaidi ya kuishi ili tufe bila kufika Uzima wa Milele. TUMUAMINI YESU YEYE NI NJIA.

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

UHURU WA MKRISTO

MAHUSIANO NA UPENDO BAINA YA MTU NA MUNGU

SADAKA YA MOYO